1 Wakorintho 5

Mwasherati Atengwe

1Kuna habari thabiti kwamba miongoni mwenu kuna uasherati unaotendeka; tena ni uasherati wa aina ambayo hata watu wasiomjua Mungu hawafanyi. Nimesikia kwamba kuna mtu anazini na mama yake wa kambo! 2Mnawezaje basi kujivuna! Badala yake mngepaswa kuom boleza. Huyo aliyefanya tendo hili afukuzwe na kutengwa nanyi. 3Japokuwa sipo nanyi katika mwili, lakini nipo nanyi katika roho. Na nimekwisha toa hukumu kuhusu huyo mtu aliyetenda jambo hili, kama vile ningekuwapo. 4Mnapokutana katika jina la Bwana wetu Yesu nami nikiwepo katika roho, na nguvu ya Bwana wetu Yesu ikiwepo, 5mtoeni mtu huyu kwa shetani, ili asili yake ya dhambi iangamizwe lakini roho yake iokolewe siku ile ya Bwana.

6Kiburi chenu hakifai. Hamjui kwamba hamira kidogo tu huumua donge lote la unga? 7Ondoeni chachu ya zamani ili mpate kuwa donge lisilo na chachu, kama mnavyotakiwa kuwa. Kwa maana Kristo ambaye ndiye Mwana-kondoo wetu wa Pasaka amekwisha tolewa kama dhabihu. 8Kwa hiyo, tusherehekee sikukuu hii, sio kwa chachu ya zamani, chachu ya nia mbaya na uovu bali kwa mkate usiotiwa hamira, wa moyo safi na kweli.

9Niliwaandikia katika barua yangu kuwa msishirikiane na waasherati. 10Sikuwa na maana kwamba msishirikiane na watu wa dunia walio waasherati, au wenye tamaa mbaya, wanyang’anyi au waabudu sanamu. Kufanya hivyo ingewabidi mtoke duniani. 11Lakini nilikuwa namaanisha kwamba msishirikiane na mtu ye yote anayejiita ndugu lakini ni mwasherati, mwenye tamaa mbaya, mwabudu sanamu, mtukanaji, mlevi na laghai. Wala msile na mtu kama huyo.

12Si kazi yangu kuhukumu watu walio nje ya kanisa. Je, si hao walio ndani ya kanisa mnaopaswa kuwahukumu? 13Mungu anawa hukumu walio nje ya kanisa. “Mfukuzeni mtu mwovu atoke kutoka katika ushirika wenu.”