2 Wakorintho 6

1Kama wafanyakazi pamoja na Mungu, tunawasihi msipokee neema ya Mungu bure . 2Kwa maana Mungu anasema: “Wakati ufaao niliku sikiliza, na siku ya wokovu nilikusaidia. Tazameni, huu ndio wakati ufaao; leo ndio siku ya wokovu.”

Matatizo Ya Paulo

3Hatutaki kumwekea mtu ye yote kikwazo ili huduma yetu isionekane kuwa na kasoro. 4Badala yake, kwa kila njia tunaon yesha ya kuwa sisi ni watumishi wa Mungu kwa kuvumilia: katika taabu, katika misiba, katika shida 5katika kupigwa, kufungwa gerezani na katika fujo; katika kazi ngumu, kukosa usingizi usiku na katika njaa; 6katika usafi wa moyo, katika ufahamu, subira na wema; katika Roho Mtakatifu na upendo wa kweli; 7katika maneno ya kweli na katika uwezo wa Mungu; kwa silaha za haki mkono wa kulia na mkono wa kushoto; 8katika utukufu na katika aibu, katika sifa na katika lawama; tukiwa wa kweli lakini tukionekana kuwa walaghai; 9tukiwa maarufu lakini tukihesabiwa kama tusioju likana; tukiwa kama wanaokufa lakini tunaishi; tukiadhibiwa lakini hatuuawi; 10tukiwa wenye huzuni lakini siku zote tukish angilia; tukionekana maskini lakini tukiwafanya wengi kuwa mata jiri; tukiwa kama wasio na kitu lakini tukiwa na vitu vyote.

11Tumesema wazi nanyi, ninyi ndugu wa Korintho, na kuweka mioyo yetu wazi kabisa kwenu. 12Sisi hatujizuii kuwapenda, bali ninyi mmeuzuia upendo wenu usitufikie . 13Na sasa nasema kama na watoto wangu: ninyi pia fungueni mioyo yenu kabisa kwetu.

Msiambatane Na Wasioamini

14Msiambatane pamoja na watu wasioamini. Kwa maana kuna uhusiano gani kati ya haki na uovu? Au kuna ushirika gani kati ya nuru na giza? 15Kuna kuelewana gani kati ya Kristo na shetani? Mwamini ana uhusiano gani na asiyeamini? 16Kuna uelewano gani kati ya hekalu la Mungu na sanamu? Kwa kuwa sisi ni hekalu la Mungu aliye hai. Kama Mungu alivyosema, “Nitaishi ndani yao na kutembea kati yao, nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu. 17Kwa hiyo, tokeni kati yao, mkajitenge nao, asema Bwana. Msiguse cho chote kisicho safi; ndipo nitawakaribisha kwangu. 18Nami nitakuwa baba kwenu, nanyi mtakuwa vijana wangu na binti zangu, asema Bwana Mwenyezi.”